Wednesday, April 4, 2012

UPIGAJI KURA TUZO ZA MUZIKI MWISHO APRILI 6

 
Afisa kutoka Kampuni ya uhakiki wa mahesabu ya Innovex, Edna Masalu akieleza juu ya utaratibu wa kupiga kura kwenye tunzo za muziki Tanzania wakati akiwasilisha mada kwenye Jukwaa la Sanaa linalofanyika kila wiki makao makuu ya BASATA. Katikati ni Lloyd Zhungu kutoka Innovex na Mratibu wa Jukwaa hilo, Agnes Kimwaga.

Na Mwandishi Wetu

Zoezi la upigaji kura kwa ajili ya kuwapata washindi wa tuzo za muziki Tanzania kwa mwaka 2012 linatarajia kufikia kikomo wiki hii huku wito ukitolewa kwa wadau wa Sanaa kuendelea kuwachagua wasanii wao.

Akizungumza kwenye Jukwaa la Sanaa wiki hii makao makuu ya Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA), Afisa kutoka Kampuni ya ukaguzi na uhakiki wa mahesabu ya Innovex ambayo ndiyo yenye jukumu la kuratibu zoezi zima la upigaji kura Edna Masalu alisema kuwa, mchakato wake unaendelea vema na unatazamia kufika kikomo wiki hii.

“Zoezi la upigaji kura lililodumu kwa zaidi ya mwezi mmoja na nusu litafikia mwisho wiki hii Aprili 6, wadau wa muziki wanahamasishwa kuendelea kuwachagua wasanii wenye kazi wanazoona ni bora katika kipindi hiki ili kuwawezesha kushinda” alisema Edna.

Kuhusu umakini kwenye zoezi la kupiga kura, Edna alisema kuwa, Kampuni ya Innovex imebuni njia mbalimbali za upigaji kura ili kuwawezesha wadau wa Sanaa wa kada mbalimbali kuweza kupata fursa ya kupiga kura na kuwa sehemu ya tuzo hizo zenye umaarufu katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

Alizitaja njia hizo ambazo zinatumika kupiga kura kuwa ni pamoja na ujumbe mfupi wa simu ya mkononi kupitia namba maalum, magazeti, vipeperushi na mitandao ya kompyuta ambapo alisisitiza kwamba, kila mtanzania ana haki ya kupiga kura moja tu kwa kila eneo (category) inayoshindaniwa.

“Hakuna njia yoyote ya upendeleo, kura zinapigwa na kuhesabiwa kwa uwazi kupitia mtandao. Toka Academy imeanza hadi sasa zoezi la upigaji kura kwa watanzania mfumo ni wa wazi na hakuna mwanya wa upendeleo” alisisitiza.

Awali, akiongea kuhusu tuzo hizo, Mratibu kutoka BASATA Angelo Luhala alisema kuwa, wasanii na wadau wa Sanaa wanapaswa kuthamini tunzo hizo kama kitu chao kwani ni kitu kilichobuniwa na watanzania kwa ajili ya kukuza muziki nchini.

“Malengo ya tuzo hizi ni kukuza muziki nchini na kuwapa ari wasanii wabuni kazi zenye ubora. Ni wazi msanii anayepata fursa ya kuwa kwenye moja ya kipengele kinachoshindaniwa ni heshima kubwa” Alisisitiza Luhala.

Tuzo za muziki Tanzania kwa mwaka 2012 zinatarajia kufikia kilele chake Aprili 14 mwaka huu kwenye Ukumbi wa Mlimani City ambapo wasanii mbalimbali watatambuliwa na kutuzwa.

Mratibu wa Tunzo za Muziki Tanzania kutoka BASATA, Bw. Angelo Luhala akisistiza jambo kuhusu tunzo hizo. Pamoja na mambo mengine alitoa wito kwa watanzania kuziona tunzo hizo kama kitu chao wanachopaswa kujivunia.

Mzee Rashid Masimbi ambaye ni moja ya wadau wanaoheshimika kwenye tasnia ya Sanaa nchini akitoa maelekezo na ufafanuzi kuhusu tuzo za muziki huku wadau wakimsikiliza kwa umakini.